Thursday, January 21, 2016

Jotoardhi ni muhimu kwa Tanzania: Kamishna wa Nishati

Kutokana na ongezeko la mahitaji ya nishati ya umeme nchini, nishati itokanayo na jotoardhi imeelezwa kuwa muhimu kwa kuwa itachangia katika kukidhi mahitaji ya nishati   ambayo ni kiunganishi kikuu cha ukuaji wa uchumi.
Akiwasilisha mada katika Kongamano la Tano la Kimataifa la Jotoardhi kwa nchi za Bonde la Ufa, lililofanyika jijini Arusha kuanzia tarehe 27Oktoba – 2 Novemba, 2014, amesema kuwa jotoardhi inaweza kuwa suluhisho la mahitaji ya nishati kwa Tanzania na dunia.
Kamishna wa Nishati na Petroli Eng. Hosea Mbise akifafanua jambo
Kamishna wa Nishati na Petroli Eng. Hosea Mbise akifafanua jambo
“Tanzania inahitaji nishati mchanganyiko ikiwemo itokanayo na jotoardhi ili kukidhi mahitaji ya nishati ya umeme nchini ambayo mahitaji yake yamekua kwa kiasi cha asilimia 12-15 kwa mwaka mmoja,” alieleza Mhandisi Mbise.
Kamishna Mbise alifafanua kuwa, hadi kufikia mwishoni mwa mwaka 2015 Tanzania itakuwa imeunganishwa na nishati ya umeme unaofikia kiasi cha megawati 3000 ambapo ifikapo mwaka 2033 kiasi cha megawati za umeme 10,000 zinatarajiwa kuzalishwa.
Alieleza kuwa, zipo fursa kwa sekta binafsi kushiriki katika shughuli za uwekezaji na uendelezaji wa nishati hiyo kutokana na uwepo wa Sera mpya ya Nishati ya mwaka 2014 ambayo imezingatia masuala ya nishati jadidifu ikiwemo jotoardhi, Sheria ya umeme ya mwaka 2008, Sera ya ushiriki wa sekta ya Umma na Sekta Binafsi ya mwaka 2009 na taratibu nyinginezo.
Kamishna Mbise alisema kuwa, Serikali itahakikisha kuwa inaendeleza nishati ya jotoardhi kutokana na mazingira bora yanayoruhusu kuendeleza nishati hiyo ikiwemo kuanzishwa kwa Kampuni ya Maendeleo ya Jotoardhi ya Taifa (TGDC), mchango wa serikali katika kusaidia masuala ya uchorongaji katika maeneo ya Ziwa Ngozi na Songwe Mkoani Mbeya, katika Ziwa Natron (Manyara), Kisaki Morogoro na Luhoi (Pwani).
Aidha, Kamishna Mbise alisema kuwa, taasisi za Kimataifa zimetoa kipaumbele cha kuendeleza jotoardhi Tanzania na Afrika zikiwemo Benki ya Dunia (WB), Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Shirika la Umoja wa Maendeleo la Japani (JICA), Shirika la Kimataifa linaloshughulikia Mazingira (UNEP) na Shirika la Misaada la Watu wa Marekani (USAID). Ameongeza kuwa ushirikiano huo na mazingira wezeshi yataiwezesha Tanzania kufikia lengo la kuzalisha megawati 200 zitakazotokana na jotoardhi ifikapo mwaka, 2020.
Imeandaliwa na:
Asteria Muhozya,
Afisa Habari,
Wizara ya Nishati na Madini,
754/33 Mtaa wa Samora,
S.L.P 2000 Dar es Salaam,
Simu: +255-22-2121606/7, Nukushi: +255-22-2121606
Barua Pepe: info@mem.go.tz
Tovuti: www.mem.go.tz

No comments:

Post a Comment